WAFANYAKAZI WIIZARA YA FEDHA WASISITIZIWA MAADILI, UBUNIFU
WAFANYAKAZI, Wizara ya Fedha wametakiwa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maadili ya Utumishi wa Umma, Sheria, Kanuni na Miongozo mbalimbali ya Serikali ili kuimarisha utawala na utoaji huduma bora kwa wananchi.
Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Fedha, Laurent Luswetula wakati akifungua rasmi Mkutano wa 39 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo kwa mwaka 2025/26 uliofanyika katika Ukumbi wa Kambarage (Treasury Square) jijini Dodoma.
Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omar, Naibu huyo alisema kuna umuhimu kwa watumishi kuwa wabunifu, kufanya kazi kwa weledi, uadilifu na ushirikiano ili kuongeza ufanisi wa huduma zinazotolewa na Wizara na kusisitiza umuhimu wa kuimarisha mifumo ya mawasiliano na mrejesho kwa wadau mbalimbali ili kuongeza tija katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali.
Luswetula, amewataka watumishi kuzingatia afya zao kwa kushiriki katika programu za upimaji wa afya zinazoratibiwa na Wizara, kufanya mazoezi ya mwili mara kwa mara pamoja na kuzingatia ushauri wa wataalam wa afya kuhusu lishe bora ili kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza.
Katika hatua nyingine, aliwahimiza wajumbe wa Baraza hilo kuwa mfano wa kuigwa katika utunzaji wa mali za umma na kuhakikisha maelekezo yote yanayotolewa na Serikali na viongozi mbalimbali yanatekelezwa kwa wakati na kwa ufanisi.
“Ninasisitiza kwamba tuendelee kufanya kazi kwa bidii, uaminifu, weledi na ushirikiano mkubwa. Kufanya kazi Wizara ya Fedha si kwa bahati mbaya, tumeaminiwa tutimize wajibu wetu. Tujiepushe na vitendo viovu, tuwe wazalendo kwa nchi yetu”, alisema Luswetula.
Aidha, aliwataka wajumbe wa Baraza hilo kusikiliza kwa umakini mada mbalimbali zitakazowasilishwa katika mkutano huo na kuzitumia kama chachu ya kuibua mawazo yenye tija kwa maendeleo ya Wizara na Taifa kwa ujumla.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha anayeshughulikia huduma za Hazina, Nsubili Joshua, alisema kuwa mkutano huo ni kwa mujibu wa Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini SURA 366 ambapo lengo lake ni kuongeza ushirikishwaji wa watumishi katika masuala mbalimbali ya Wizara.
Alifafanua kuwa kikao hicho kimewajumuisha wajumbe 222 kutoka katika Chama cha Wafanyakazi, Menejimenti ya Wizara, Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya wizara na wawakilishi kutoka katika Idara na Vitengo.
Joshua ameeleza kuwa Mkutano huo ni jukwaa muhimu la kujadili masuala ya ustawi wa watumishi, kuimarisha uhusiano kazini na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara.
Aidha, alibainisha kuwa katika kikao hicho wajumbe watapata nafasi ya kusikiliza na kuchangia mada mbalimbali zilizowasilishwa kwa kuzingatia ratiba iliyotolewa pamoja na kushiriki katika majadiliano ya masuala mbalimbali yanayolenga kuboresha utendaji kazi wa Wizara.
Wakati wa mkutano huo, ulifanyika uchaguzi wa kumteua Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo na Ramadhani Kipambe alishinda uchaguzi huo.







Comments
Post a Comment