UJIO WA KAGAME, RUTTO AIBU KWA MAKUWADI WA KISIASA E.A-MBETO


Na Mwandishi  Wetu, Zanzibar 

Chama Cha Mapinduzi  (CCM), kimetaja ziara za Rais wa Rwanda na wa Kenya  nchini ni majibu tosha kwa   wanasiasa na wanaharakati kiliowaita uchwara,  wanaojihusisha na ukuwadi wa kisiasa Afrika Mashariki.

Hivyo basi,  CCM kimewataka  wana Afrika Mashariki wote kupuuza  uvumi  usio na mashiko ukidai Mataifa  E.A  hayana uhusiano Mwema. 

Matamshi hayo yametamkwa na Katibu  wa Kamati  Maalum ya  NEC  Zanzibar, Idara ya Itikadi, Uenezi  na Mafunzo, Khamis  Mbeto Khamis ofisini kwake Kisiwandui Visiwani Zanzibar.

Mbeto alieleza hayo mara baada ya Marais hao kuitembelea   nchi huku akieleza kuwa  uhusiano wa Tanzania kidiplomasia  wa Kikanda na Kimataifa, hautadhoofika.

Mbeto alisema  wapo baadhi ya  wanasiasa na wanaharakati uhwara E.A ambao uelewa wao ni hafifu katika Uongozi, siasa na  utawala,  hueneza taarifa hasi zikidai Tanzania haina Uhusiano mzuri na Nchi jirani. 

Alisema Tanzania itaendelea kufuata kanuni, taratibu, misingi ya Uongozi, utawala wa sheria bila kukiuka kanuni za kidiplomasia  na kwamba  itaheshimu miiko na kanuni ili kudumisha umoja  na ushirikiano. 

"Wako wapi  wanasiasa na Wanaharakati viherehere  wakaanga sumu,   chuki na uongo. Zara za Rais Paul Kagame na  Dkt. William Rutto zimewatia aibu  makuwadi wa kisiasa na wapika  majungu Afrika Mashariki" alisema Mbeto.

Katibu Mwenezi huyp alisema Tanzania na jirani zake, washirika  wa maendeleo, wawekezaji, Jumuiya ya Afrika Mashariki na,Jumuiya za kikanda na  Mashirika ya Kimataifa, zitaendeleza  ushirikiano usio na shaka. 

"Mataifa  yetu yatizame  mbele na  kuanzisha miradi ya kiuchumi itakayotanua wigo wa ajira na  uwekezaji.

Tungependa kuziona sekta za  mawasiliano, usafiri na biashara  zikiimarika Tanzania daima  haitatikiswa na kelele wakaanga sumu " alieleza. 

Pia Mbeto  alisema kwa miaka  mingi Tanzania  imekuwa ikifanyakazi kwa ushirikiano na nchi zote jirani , hivyo uchonganishi  wenye  lengo la kuchochea  mitafaruku,  idhibitiwe mapema  kwa nguvu  ya pamoja. 

"Tusingoje hadi  hatari ishamiri  ndipo udhibiti ufanyike. Tulinde mipaka yetu kwa nguvu na sauti  moja. Uchonganishi na Uchochezi udhibitiwe ili usidhoofishe   umoja, amani  na maendeleo" alisisitiza Mbeto.

Mwenezi huyo  akizungumzia nafasi ya  demokrasia, uwazi na Utawala bora, alisema   wananchi wamepewa uwanja mpana wa ushiriki wa  demokrasia inayozingatia  nidhamu, miiko  na utii wa sheria.

'Serikali  zimetoa nafasi pana ya Utekelezaji wa  demokrasia shirikishi na si  demokrasia  holela. Serikali zetu zinaheshimu  sheria, uhuru wa Kijamii wenye mipaka kwa mujibu wa sheria na katiba "   alisema Mbeto.

Comments

Popular posts from this blog

CCM YAISHUKURU SMZ, WAKAZI KIKWAJUNI

CCM YAONYA WATEULE MIUNDOMBINU ZANZIBAR

TRA YATAKIWA IJIPANGE DIRA MAENDELEO YA TAIFA