MBETO: WANASIASA WASTAAFU WACHAMBUZI LINDENI MASLAHI YA TAIFA
Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimewataka viongozi wa siasa wastaafu, wanataaluma, wasomi wabobezi na wachambuzi wa masuala ya kisiasa, kijamii na kiuchumi kutambua kuwa kubomoa Taifa ni rahisi kuliko kulijenga.
Pia ametaja kauli au maneno yanapotolewa bila tafakuri ya kina mara nyingi huzua sintofahamu na kusababisha uvunjifu wa amani.
"Ukiichezea amani ni sawa na kuchezea upanga wenye makali au kuwasha moto kwenye nyasi kavu hivyo kusambaa na kuleta maafa makubwa" alisema Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya Itikadi Uenezi na Mafunzo , Khamis Mbeto Khamis.
Mwenezi huyo alisema kumezuka tabia za hivi karibuni za baadhi watu kutamka maneno bila kupima athari na faida zake katika jamii yenye watu waungwana .
"Tabia ya baadhi ya viongozi Wastaafu kutoa maneno makali bila kuyapima ni hatari. Pia kuna baadhi ya wasomi na wanataaluma wanaoheshimika hutamka maneno ya kuogofya. Wajue tu maneno makali hubomoa badala ya kujenga nchi" alisema Mbeto
Katibu huyo Mwenezi alisema ipo haja ya kujadiliana mambo kwa kufuata taratibu zinazofaa ambazo haziachi athari katika jamii lakini pia si uungwana watu wazima wakawa na sifa ya kusema sema hovyo kila uchao ili kutaka sifa ya utukufu.
Mbeto aliwataka Watanzania kujua thamani ya Umoja wao kuliko hasara ya kutoa maneno yanayopandikiza chuki, hasama na uasi katika jamii.
"Wananchi, wastaafu, wasomi, wachambuzi na wanataaluma wanapaswa kuwa wa kwanza kuitakia mema Tanzania" alisema Mwenezi Mbeto.
Alibainisha kuwa watakao ifikisha Tanzania miaka mingine sitini Taifa likiwa moja ni watanzania wenyewe.
"Ni kosa mtu kufikiri yatakapozuka majanga au machafuko ana uhakika wa kubaki salama. Fujo, ghasia na vurugu hazina macho wala masikio, huwadhuru matajiri, masikini, viongozi na raia wema wasio na hatia bila kutarajia" alisema.
Aidha Katibu Mwenezi huyo alisema hakuna gumu lisiloweza kuzungumzika na kumalizwa kwa njia za kiungwana., hivyo aliwashauri maneno yao yawe ya kulinda umoja wa Kitaifa.
"Wapo baadhi ya wenzetu wanataka kutumia fujo na vurugu kama mtaji wa kushika madaraka. Huwezi kupata utawala kwa mbinu hizo batili. Njia pekee inayokubalika ni demokrasia ya uchaguzi ili kushika uongozi badala ya kususia " alisisitiza Mbeto.

Comments
Post a Comment