MBETO: OMO MPOTOSHAJI, UCHAGUZI MKUU ZANZIBAR UMESHAPITA
Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimemtaka Mwenyekiti wa ACT Wazalendo , Othman Masuoud Othman 'OMO' kutowapotosha wananchi kwa kudai kuna waliojipa mamlaka wakati kura zilizopigwa ndizo zilizoiweka serikali madarakani.
Katibu wa Kamati Maalum NEC, Zanzibar Idara ya Itikadi na Uenezi, Komredi Khamis Mbeto Khamis alisema
kwa muktadha huo, CCM kimesikitishwa kumsikia kiongozi huyo akipotosha ukweli kuhusu Uchaguzi Mkuu uliopita.
Mbeto alisema kauli ya kiongozi huyo ni kama kwamba uchaguzi bado haujafanyika Zanzibar.
Mwenezi huyo alidai kuwa matamshi ya Mwenyekiti huyo wa ACT Wazalendo yana upungufu na walakin.
"Wakati akifungua kikao cha Kamati Kuu ya ACT Wazalendo Jijini Dar es Salaam, Othman alidai kuna waliojipa madaraka huku wakishindwa kutenda haki na kutotimiza wajibu stahiki kwa wananchi" alisema Komredi Mbeto.
Alibainisha kuwa hakuna Serikali Duniani inayojiweka Madarakani bila kupata ridhaa na idhini ya wananchi kupitia ushiriki wao katika demokrasia ya uchaguzi.
Alisema jaribio la kutaka kuiaminisha jamii na Dunia ya kwamba Serikali iliyopo imejiweka madarakani ni upuuzi unaopaswa kupuuzwa.
"Hizo ni Ngenga , Varange na sarakasi za kisiasa, jeuri na ukaidi usio na maana wala mantiki" alitanabaisha mwenezi huyo ambaye chama chake ndio kinaunda serikali.
Komredi Mbeto alisema ACT na CCM vyote vimeshiriki Uchaguzi Mkuu 2025, Dunia nzima ikishuhudia na wagombea Urais, Ubunge, Uwakilishi na Udiwani wa Vyama vyote waliomba kura wakapigiwa.
"Chama kilichoshinda kilitangazwa na Tume ya Uchaguzi Zanzibar hivyo ni makosa kudai kuna waliojiweka Madarakani"alisma Mbeto.
Katibu Mwenezi huyo alisema CCM imekiita kitendo cha Othman kupita akidai mshindi amejiweka madarakani, madai hayo ni porojo na pambio zisizo na uzito wowote .
"Wenzetu kwa kutojua na kutaka kuendekeza malumbano majukwaani wamekuwa wakibeza maendeleo yanayofanyika ambayo wananchi kwa macho wanayaona mbaya zaidi bila wao kushiriki kutokana na kusua sua kwao kushiriki katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa" alisema na kuongeza kuwa bezo hizo zinawafanya wazidi kuporomoka kisiasa.
Mbeto alimtaka Othman akubali ukweli hakuwa na nguvu za kisiasa za kumshinda mgombea Urais wa CCM, Dkt. Hussein Mwinyi, ambaye tayari ameleta maendeleo yaliyowaridhisha wananchi miaka mitano iliopita .
"Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 umeshafanyika na matokeo yametangazwa, kukaa na kudhani Uchaguzi Mkuu bado haujafanyika ni kujidanganya mwenyewe. Uchaguzi umekwisha , mshindi amepatikana na ameshaunda serikali" alisema mwenezi Mbeto.


Comments
Post a Comment