MBETO: DEMOKRASIA YA VYAMA VINGI 'ISILIPASUE' TAIFA


                                          Na Mwandishi  Wetu, Zanzibar 

Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeviasa Vyama vya Upinzani na kuvitaka vielewe maana ya  demokrasia ya Vyama Vingi si kuizuia Serikali isitimize wajibu wake au ihofie kuchukua hatua za Kisheria pale itakapobidi.

Kadhalika CCM kimeutaja ushindani wa kisiasa ikitaka uwe ni mchuano wa hoja  na sera, si kukithiri matusi au kupandikiza  hasama na chuki.

Hayo yametamkwa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC  Zanzibar,  Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Komredi Khamis Mbeto Khamis, Zanzibar leo 11 Mei 2026.

Mbeto ambaye yuko katika Msafara wa ziara inayoendelea ya Makamu Mwenyekiti  wa CCM Zanzibar, Rais Dk Hussein Ali Mwinyi, alisema inashangaza kwa baadhi ya viongozi wa upinzani  , wakisikika katika hotuba zao zikihamasisha hasama kwa lengo la  kulipasua au  kuligawa Taifa 

"Ushindani wa siasa za chuki, hasama na matusi si kielelezo cha ustaarabu wa  kisiasa. Tunawaonya wenzetu waache siasa zisizo na  manufaa kwao, kwetu na kwa jamii yetu kwa ujumla" alisema Mbeto.

Pia Katibu  Mwenezi  huyo alisema tabia ya  baadhi ya wanasiasa kutoa vitisho au madai  yasio na ushahidi, hakuthibitishi kupevuka kwao badala yake  wananchi huwapuuza.

"Huwezi  kubagaza utu  na heshima ya  wenzako kisha uachwe  ukitamba mitaani. Vyombo vya dola na vya kisheria vipo makini. Kutuhumu wenzako kwa masuala yasio na   ushahidi si uungwana" alisema Mwenezi huyo.

Alibainisha kuwa siasa ni ushindani wa kimantiki unaoshindanisha  hoja na sera, na inaeleweka kuwa  kazi ya upinzani ni kufichua uovu ndani ya utawala lakini kuwe na  ushahidi na vielelezo si kutamka matusi  mbele ya jamii.

"CCM haijawahi kuhofia  upinzani toka mwaka 1992. Walikuwepo kina  Mabere Marando, Chifu Fundikira, Mapalala, Maalim Seif, Oscar Kambona  na Mzee Mloo ambao hawakuwatusi watu, walitoa hoja na kujibiwa kwa nguvu ya  hoja" alitanabaisha Komredi Mbeto.

Aliwataja  waasisi hao wa mfumo wa vyama vingi na kubainisha kuwa walikuwa  wamekomaa na wajenzi wa hoja makini na waliojua  umuhimu wa   amani na umoja  bila kutoa vitisho au kueneza chuki za kisiasa.

Mbeto akirejea kauli ya Makamu Mwenyekiti wa CCM na Rais  wa Zanzibar kuhusu Serikali ya Ùmoja wa kiTaifa na mazungumzo ya kusaka muwafaka, alisema ipo wazi na ndio msimamo wa CCM kuwa ipo tayari kwa Serikali hiyo ambayo ipo kisheria kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar

Mwenezi huyo alienda mbali zaidi kwa kueleza kuwa kama kuna mazungumzo yatakuwa ni juu ya mambo yanayo husiana na Sheria iliyounda Serikali  ya Umoja wa kiTaifa na kama kutakuwa na ambayo hayapo sawa, yatahitaji maamuzi ya mamlaka husika kama Baraza la Wàwakilishi  na vyombo vingine vilivyowekwa na Katiba ya Zanzibar na Sheria zake.

"Huwezi kutaka mambo ambayo kwa mujibu wa Katiba yapo kwenye mamlaka ya Rais" alisema Mwenezi huyo.

Comments

Popular posts from this blog

CCM YAISHUKURU SMZ, WAKAZI KIKWAJUNI

CCM YAONYA WATEULE MIUNDOMBINU ZANZIBAR

TRA YATAKIWA IJIPANGE DIRA MAENDELEO YA TAIFA