MBETO: CCM TUNAMPONGEZA DKT. MWINYI KUKATAA KUVUNJA KATIBA ILI ABAKI MADARAKANI ZANZIBAR
Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimepongeza uamuzi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa kushinda majaribu ya wapambe walioanza kumshinikiza avunje katiba na kuongeza muda wa kubaki Madarakani Zanzibar.
CCM kimesema ni fedheha kwa wapambe na mashabiki walioanza kumshawishi kiongozi huyo abaki madarakani kinyume na Katiba ya CCM na ya Zanzibar ya mwaka 1984.
Pongezi hizo zimetolewa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamis Mbeto Khamis kufuatia kauli ya Rais Dkt. Mwinyi aliyoitoa 22 Mei 2026 akifungua Mkutano wa Jukwaa la Watendaji Wakuu wa Taasisi la Zanzibar Chairpersons & CEO's Forum kuwa anasikia mjadala mitaani na kwenye Baraza la Wawakilishi wakimtaka aongeze muda wake madarakani jambo ambalo amelikemea na kutaka mjadala huo ukome kwani hauna tija.
Alibainisha Dkt. Mwinyi kuwa aliapa kuilinda Katiba ya Zanzibar hivyo hayupo tayari kuifanya vingine na kuhoji kusudio la hao wanaotaka aongoze muda kinyume na Katiba ya Zanzibar.
Mwenezi Mbeto alisema huo ndio uamuzi na msimamo wa CCM kuwa kwa mujibu wa Mila na Utamaduni wa CCM, matakwa ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 na Katiba ya CCM, Rais atakaa madarakani vipindi viwili kwa miaka kumi na hatawania tena nafasi hiyo.
Alisema matamshi yaliotamkwa na baadhi ya wapambe kwa utashi wao binafsi ni dhamira batili, kwani hakuna Rais kupitia CCM anayeweza kupata nafasi ya kuongeza muda wa kubaki madarakani kinyume na taratibu.
"Hata iweje kwa Rais aliye Madarakani akitokea ameleta maajabu ya kiutendaji katika kusimamia maendeleo, muda wake kikatiba utabaki kuwa ule ule wa miaka kumi madarakani. Kila Rais akimaliza miaka hiyo atawapisha wengine" alisema Mbeto.
Katibu Mwenezi huyo aliliita tangazo la Rais Dkt. Mwinyi kukataa kubaki Ikulu ifikapo mwaka 2030 na kwamba hana fikra wala mpango wa kuongeza muda ili abaki madarakani ni aibu kwa walioanza kumshabikia.
"Kiongozi yeyote muungwana uheshimu Katiba aidha ya chama au nchi. Kuvunja ahadi na miadi au kufanya kinyume chake hiyo ni dalili ya kiongozi huyo kukosa utu na ustaarabu" alisisitiza.
Mbeto alisema Tanzania hususan ndani ya CCM, kuna wanachama wengi wenye uwezo wa kubeba dhamana ya Urais na kuitumikia nchi kwa uzalendo, uadilifu na uaminifu, hivyo nafasi ya kiongozi mmoja kubaki madarakani milele haipo.
"Nafasi zaidi ya miaka mitano ilitolewa kwa Waasisi Wetu Mwalimu Julius Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume. Baada ya wao hatatokea yeyote wa kuongeza muda zaidi ya kuongoza aidha kwa Zanzibar au kwa Tanzania" alieleza Mwenezi Mbeto.

Comments
Post a Comment