CCM YAIPONGEZA SMZ KUONGEZA KIMA CHA CHINI CHA MSHAHARA
Na Mwandishi wetu, Zanzibar
Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeipongeza kwa dhati Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), chini ya Rais Dk Hussein Ali Mwinyi kwa kupandisha mshahara kima cha chini kutoka TSh.300,000 hadi TSh.500,000 kwa mwezi.
CCM kimeitaka SMZ kuendelea mkakati wa kutazama hali za maslahi ya wafanyakazi wa kima hicho ili waweze kustawi na kujijenga kiuchumi.
Hayo yameelezwa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamis Mbeto Khamis mara baada ya SMZ kutangaza kima kipya cha mshahara wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi, visiwani humo.
Mbeto alisema ongezeko hilo la mshahara kwa kima cha chini ni fursa nyingine kwa wafanyakazi itakayosaidia katika kustawisha maisha yao.
Komredi Mbeto alisema mshahara huo mpya bila shaka SMZ imezingatia hali ya uchumi na maisha ya kila mZanzibari, gharama za maisha na kuwapa motisha wafanyakazi, wazidi kusimamia majukumu yao kwa ufanisi.
'Siku zote motisha huongeza tija kazini. Tunawahimiza Wafanyakazi wote katika taasisi za umma, Wizara, Idara na sekta zote wakasimamie nidhamu ya kazi ili kuongeza kasi ya uzalishaji" alisema Mbeto
Aidha, alitoa kongole kwa uongozi wa SMZ Awamu ya Nane kwa kujali na kutazama na kuinua hali za wananchi ikiwa ni sehemu ya utekelezaji ahadi za kisera na ahadi binafsi za Rais Dkt. Mwinyi.
"Tokea aingie madarakani Rais Dk Mwinyi hii ni mara ya pili kupandisha mshara kima cha chini. Anafanya haya yote kwa kujali watu na maisha yao. Uungwana wa mtu ni kutenda si kusema maneno matupu" alibainisha Mbeto.
Pia Mwenezi huyo alisema CCM kitaendelea kuzishauri mara kwa mara serikali zake ili zihakikishe maisha ya wananchi yanakimbizana na hali halisi ya kiuchumi.

Comments
Post a Comment