MBETO ABAINISHA DUNIA ISIVYO NA SHAKA NA DEMOKRASIA YA TANZANIA


                                          Na Mwandishi  Wetu, Zanzibar 

CHAMA cha Mapinduzi (CCM), kimejinasibu kuwa Tanzania  inafuata na kutekeleza aina bora ya demokrasia   chini ya uongozi wa chama hicho, kutokana na upana wake,  ushiriki wa wananchi  na uwazi usiotiliwa  shaka. 

Pia chama hicho  kimesema kiwango cha ukosoaji, michango, fikra na maoni  jumuishi ya wananchi  husikilizwa,  kutekelezwa na medani za utawala.

Hayo yametamkwa na Katibu wa Kamati  Maalum ya NEC  Zanzibar, Idara ya Itikadi, Uenezi  na Mafunzo, Komredi Khamis Mbeto Khamis  aliposhiriki hitimisho la Mdahalo wa Muungano  ulioandaliwa na  Chuo Kikuu  cha Taifa (SUZA), kupitia Kigoda cha Taaluma cha Sheikh Abead Amani Karume.

Mbeto  alisifu uwamuzi wa viongozi wa Mataifa ya Tanganyika na Zanzibar  kwa kutanguliza kwao maslahi mapana ya Taifa kwa kuwaunganisha Wananchi miaka  62 iliopita.

Aidha alisema kiwango cha  aina ya demokrasia iliopo nchini,   kinatokana na  ustawi wa uhuru wa wananchi.

Nafasi pana ya ukosoaji, utoaji maoni, ushauri huku wakipata maelezo toka serikalini.

Mbeto alisema ni nchi chache sana  duniani zenye kufuata  mfumo wa demokrasia   inayolingana na  utaratibu uliopo Tanzania

 "Abadan sina shaka na aina ya demokrasia yetu Tanzania. Tuna ustawi mkubwa wa  demokrasia  iliovuka mipaka.

Leo kuna wanaofika hadi kutukana viongozi bila sababu hawakamatwi. Ni  demokrasia yenye rutuba,  kinga na Uvumilivu" alisema Mbeto.

Katibu huyo Mwenezi  alisema ni nadra kuikuta aina ya demokrasia hiyo katika Mataifa mengine kama ilivyo Tanzania,  lakini  yote hiyo imetokana na  dhima ya ukomavu wa kisiasa, uvumilivu, ujenzi mpya wa Taifa, mapatano na maridhiano.

Akijibu swali kuhusu msimamo wa chama chake wa kuandika katiba mpya, alisema kabla Rais Dk Samia Suluhu Hassan hajamaliza muda wake madarakani kikatiba, serikali yake itawapatia WaTanzania Katiba Mpya.

"Wakati Dkt. Samia alipokuwa akizindua kampeni ya Uchaguzi Mkuu wa  chama chetu  katika Viwanja vya Tanganyika Peckers,  amewaahidi  WaTanzamia Serikali yake itawapatia Katiba mpya" alisema.

Kadhalika Mbeto  alisema ajenda ya Katiba mpya ni ya Serikali za CCM,  si ya upinzani. Tume zote za Ukusanyaji maoni ya wananchi  zimeundwa  na serikali zilizopo madarakani. 

"Itaandikwa  Katiba mpya itakayozingatia ushauri na maoni yote ya wananchi. Itapitia na kuzingatia mapendekezo ya Tume za Jaji   Nyalali, Jaji Kisanga, Jaji  Warioba na Jaji  Chande"  alisisitiza.

Hata hivyo, mwenezi huyo alisema  Katiba mpya itafuata   ushauri  uliotolewa na wananchi, kulinda tunu za Taifa ustawi wa kisiasa, uboreshaji mifumo ya Uchaguzi na kuwashrikisha  wadau wa maendeleo ya demokrasia.

Comments

Popular posts from this blog

CCM YAISHUKURU SMZ, WAKAZI KIKWAJUNI

CCM YAONYA WATEULE MIUNDOMBINU ZANZIBAR

TRA YATAKIWA IJIPANGE DIRA MAENDELEO YA TAIFA