HEMEDI: TUMIENI KIPINDI HIKI KUKIJENGA CHAMA
VIONGOZI wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Zanzibar wametakiwa kukitumia kipindi hiki kukijenga chama ili ifikapo 2027 kwenye chaguzi za ndani wakachague viongozi kwa ajili ya maslahi ya chama na sio mtu.
Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo yaliyoratibiwa na Ofisi ya Naibu Katibu Mkuu, Idara Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Ofisi Kuu Kisiwandui Unguja, Mjumbe wa Kamati Kuu Halmashauri Kuu CCM Taifa, Hemed Suleiman Abdula ambaye pia ni Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, alisema mafunzo waliyopata yatawasaidia kuwaweka karibu zaidi katika kutimiza wajibu wao wa kimsingi uliowapa nafasi za uongozi.
"Chama chetu kinaelekea katika uchaguzi, sikuwepo lakini najua mtakuwa mmelizungumzia hili na hongereni kwa kazi nzuri" alisema.
Alisema ni jambo kubwa viongozi kuelewana na kukaa pamoja na kukumbushana wajibu wao na kupata mafunzo ni jambo moja na kutekeleza yale waliyojifunza ni jambo la pili.
Mjumbe huyo wa Kamati Kuu aliwaomba viongozi hao wakayatekeleze waliyojifunza na wakifanya hivyo wataweza kufanya vizuri wakati wote katika kukitetea chama.
Mjumbe Hemed Suleiman Abdulla, alimshukuru Mwenyekiti CCM pia Ofisi ya Makamu Mwenyekiti anayefanyia shughuli zake Zanzibar kuridhia kufanyika kwa mafunzo hayo na kutoa ushirikiano mkubwa.
"Shukrani ndugu yangu Mbeto kwenye Idara ya Mafunzo, tunashukuru kweli, kweli" alisema Hemed na kuongeza kuwa ni jambo kubwa nao watazidi kujifunza kuhakikisha chama kinazidi kuwa imara.





Comments
Post a Comment