VYUO VYA UDEREVA ZANZIBAR VYAPEWA MUDA KUJIBORESHA

                                    Na Mwandishi Wetu, Zanzibar

NAIBU Waziri wa Ujenzi na Uchukukuzi, Badriya Atai Masoud, ameviagiza vyuo vya Mafunzo ya Udereva Zanzibar kuchukua hatua za haraka kurekebisha kasoro zilizoainishwa, wakati alipofanya ziara ya kushtukiza katika vyuo hivyo mbalimbali vya udereva akiwa na mamlaka za usalama barabarani.

Akizungumza mara baada ya ziara hiyo ya kusikiliza changamoto zinazovikabili vyuo hivyo na kutafuta njia ya bora ya kufuata, Naibu Waziri Badriya alisema wamegundua mapungufu kadhaa katika baadhi ya vyuo.

"Tumegundua mapungufu kadhaa ikiwa ni pamoja na ukosefu wa vifaa muhimu vya kufundishia" alisema na kuvitaja kuwa ni pamoja na mashine ya kupoza injini ya gari (Radiator), mfumo wa breki, Injini, mfumo wa mneso kwenye gari (Shockabsover), Mfumo wa mtengamano wa gari (Stabilizer) pamoja na ukosefu wa michoro sahihi kwenye viwanja vya mazoezi ya udereva.

"Tumebaini baadhi ya viwanja  vya kujifunzia havikidhi vigezo na mahitaji kwa ajili ya kutoa mafunzo bora ya udereva" alisema Naibu Waziri Badriya ambaye pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Kijini.

Alisema wamewataka wamiliki wa vyuo hivyo kuchukua hatua za haraka kurekebisha hali hiyo na kushindwa kufanya hivyo kutailazimu serikali kuchukua hatua za kisheria ikiwemo kusimamisha shughuli za vyuo husika au kufuta usajili wake.


Naibu huyo ambaye alikuwa akimwakilisha Waziri wake kwenye zara hiyo ya kushtukiza alisema imetokana na ongezeko la ajali za barabarani na serikali inaendelea kuchukua hatua madhubuti kutathmini na kubaini vyanzo vya matatizo.

Alibainisha kuwa lengo ni kuweka mikakati madhubuti itakayo saidia kupunguza ajali na kuimarisha usalama barabarani kwa manufaa ya wananchi wote.


Wamiliki wa vyuo hivyo licha ya kuishukuru serikali kwa ushirikiano wameomba kuongezwa kwa wasimamizi wa mitihani ya vitendo (kwa silva) ili kurahisisha na kuharakisha utoaji wa huduma hiyo kwa wanafunzi wa udereva.



Comments

Popular posts from this blog

CCM YAISHUKURU SMZ, WAKAZI KIKWAJUNI

CCM YAONYA WATEULE MIUNDOMBINU ZANZIBAR

TRA YATAKIWA IJIPANGE DIRA MAENDELEO YA TAIFA