MBETO 'AMPASHA' OMO SIASA ZA HASAMA ZANZIBAR

 

Na Mwandishi Wetu, Zanzibar 

Chama cha Mapinduzi (CCM), kimemtaka Mwenyekiti  wa ACT Wazalendo  Othman Masoud  Othman kuacha porojo na kuwapotosha wananchi kwa kupandikiza maneno  ya hasama na chuki  katika jamii huku akiahidi mambo  yasiowezekana.

Vile vile,  CCM kimesisitiza kuwa Uchaguzu Mkuu 2025 umemalizika, wananchi  wametumia haki yao ya kikatiba na kidemokrasia kwa kuiweka Serikali  walioitaka  madarakani.

Matamshi hayo yametamkwa na Katibu wa Kamati  Maalum ya NEC  Zanzibar, Idara ya itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamisi  Mbeto Khamis aliyemtaka Othman kukubali ukweli    ameshindwa  uchaguzi kutokana na nguvu ya maamuzi ya wengi.

Mbeto  alisema  Othman hana sababu zenye mashiko, bali  anajaribu  kuidanganya Dunia akidai  yeye ndiye mshindi wakati Tume  ya Uchaguzi  Zanzibar (ZEC), imeshamtangaza mgombea aliyeshinda Urais.

Alisema Othman  asingeweza kumshinda mgombea wa CCM, Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa sababu kadhaa muhimu ambazo   zina ukweli usiokwepeka.

"'Othman alikuwa akiomba nafasi ya kuchaguliwa ili awatumikie wananchi wa Zanzibar. Rais  Dk  Mwinyi alishapimwa jinsi  ilivyoitumikia  nchi na watu  miaka mitano iliopita.  Ndoto  ya OMO ni kuleta maendeleo wakati mwenzake alishafanya kazi  ya kuleta   maendeleo inayoonekana"  alisema Mbeto.

Katibu  huyo Mwenezi  alisema fikra na hesabu za Othman, alidhani wananchi  wangembagua na kumchukia Rais Dkt. Mwinyi kutokana na matamshi ya Makamu wake Mwenyekiti,  Ismail Jussa Ladhu alivyokuwa akitumia hotuba za ubaguzi kama sera na mtaji wa kupata ushindi.

"Zanzibar nchi ya visiwa. Ni mkusanyiko na mkutanisho wa watu toka pembe nyingi za Dunia, anapoonyesha au chama chako kina sera za kibaguzi unalazimisha upigiwe kura za chuki dhidi yako" alieleza.

Pia Mwenezi huyo alisema miaka mitano iliopita utawala wa Rais  Dkt. Mwinyi  umewaunganisha wananchi  waliogawanyika kwa siasa za chuki. Ameongoza bila kujali asili zao, rangi walizonazo, siasa au itikadi  za  vyama vyao.

"Kwa miaka mitano iliopita  Wazanzibari  waliishi kwa utulivu kama maji ndani ya mtungi. Wamekuwa wamoja, wenye  upendo mshikamano. Hazikusikika sauti za kubaguana, kusimangana wala kuhitilafiana "alisisitiza.

Mbeto alimtaja Jussa kuwa ndio kiongozi pekee  ambaye  kila wakati alisikika  katika mikutano  yake akijaribu kuwagawa wananchi asili, nasaba na siasa ili kuwavuruga kwa historia na   matukio ya kisiasa yaliopita. 

"Kushindwa kwake OMO kwa sehemu kubwa kumeporomoshwa na aina ya utata wa siasa na matamshi ya Jussa. Wazanzibari wamechoshwa na heka heka za kubaguana na kugombanishwa kwa itikadi za vyama" alisema Mwenezi huyo.

Comments