DKT. NCHIMBI KUWEKA JIWE LA MSINGI TAWI UDSM BUKOBA
DKT. NCHIMBI KUWEKA JIWE LA MSINGI TAWI UDSM BUKOBA
Na Mwandishi Wetu, Bukoba
MAKAMU wa Rais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Emmanuel Nchimbi anatarajiwa kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa tawi la Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), 15 Desemba 2025.
Akizungumza na wanahabari ofisini kwake Mjini Bukoba, Mkuu wa Mkoa wa Kagera Hajjat Fatma Mwassa alisema chuo hicho kitajengwa Kijiji cha Itahwa, Kata ya Kalagabaine, Halmashauri ya Mji wa Bukoba.
Alisema Dkt. Nchimbi katika uwekaji wa jiwe hilo la msingi ataambatana na Mkuu wa Chuo Kikuu Dar es Salaam, Rais mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.
Alisema ujenzi wa chuo hicho ni sehemu ya mpango wa serikali kupanua wigo wa upatikanaji wa elimu na kufungua fursa za kiuchumi kwa wenyeji na vitongoji vyake na kuwataka wananchi kuchangamkia fursa hiyo muhimu.
Awali akizungumza wakati wa mkutano huo, mratibu wa ujenzi wa chuo hicho, Profesa Liberato Haule alisema awamu ya kwanza ya ujenzi wa chuo hicho 2026/2027 utahusisha majengo yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 800.
“Chuo awamu ya kwanza kitapokea wanafunzi 660 na matarajio ifikapo 2030 kiwe na uwezo wa kuwahudumia wanafunzi 1,600” alisema.
Alibainisha kuwa chuo kitakuwa mchepuo wa biashara na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kutakuwa na kituo cha ushauri kwa wafanyabiashara.

Comments
Post a Comment