DKT. MWINYI; ZSSF WEKEZENI MIRADI YA UMEME








 Mwandishi Wetu, Zanzibar

RAIS wa Zanzibar  na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Ali Mwinyi angependa kuona Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya  Jamii Zanzibar (ZSSF), ikiwekeza kwenye miradi mikubwa zaidi ikiwemo ya umeme.

Alizungumza wakati wa kuzindua nyumba  za kisasa za bei nafuu  zilizojengwa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar  (ZSSF), leo 23 Desemba 2025, eneo la Mombasa, Unguja zilizopewa jina la 'Mji wa Rais Hussein Mwinyi'.

Dkt. Mwinyi, alisema kuwa mifuko ya hifadhi ya jamii inatekeleza miradi mikubwa ulimwenguni.

Alisema  ni vema wakajifunze nchi zingine wanafanyaje na akatoa mfano wa Malaysia, Singapore na Indonesia ambako miradi  yote mikubwa ya maendeleo inafanywa  kwa  uwekezaji wa mifuko ya jamii.

"Mfano hivi sasa  Zanzibar kuna changamoto kubwa ya umeme hivyo ningependa  kuona mkiwekeza   kwenye miradi mikubwa ya maendeleo kama hiyo" alisema.

Alibainisha kuwa  kukamilika kwa mradi huo wa nyumba 76 za makazi na biashara ni mwanzo mzuri kwa ZSSF kuelekea miradi mikubwa zaidi.

"Ukiacha jukumu la msingi la mifuko ya hifadhi ya jamii kutunza maslahi  ya watumishi hadi wanaostaafu  licha ya  kazi kubwa zinazofanywa na mfuko  za kujenga masoko, stendi, vituo vya mabasi kwanini msiwekeze kwenye umeme" alihoji Dkt. Mwinyi.

Alisema serikali inaposema inaenda  kuacha alama basi iwe kubwa itakayodumu na amehidi kuibadilisha Zanzibar kwa kuwajengea  wananchi nyumba  bora  za  kisasa  na kuwaondoa kwenye mazingira duni.

Alitaja maeneo ya Michenzani, Kilimani, Kikwajuni, Jang'ombe kote ni  maeneo ambako wakazi wake wengi wanaishi katika nyumba duni na ndoto  yake ni kuiona Zanzibar mpya yenye mazingira mazuri ya kuishi wananchi.

Alibainisha kuwa  walio wengi wanaishi maeneo yasiyopimwa, hakuna barabara wala njia za majimachafu jambo ambalo alisema halikubaliki na Zanzibar  inatakiwa  iwe  na miji mipya  ya kisasa yenye  mazingira mazuri kwa wananchi.

Nyumba hizo zenye uwezo wa kutosheleza ukubwa wa familia tofauti kila ghorofa lina sehemu ya bustani ya kupumzikia, viwanja vya kuchezea  watoto, maegesho ya magari kwa wenyeji na wageni, mfumo wa kuondoa majitaka hadi mtaro mkuu, msikiti na maduka ya biashara.

Mpaka uzinduzi unafanyika, asilimia 87 ya nyumba hizo tayari zimeuzwa.

Kuelekea kilele cha Maadhimisho  ya Siku ya Mapinduzi, Rais  Dkt. Mwinyi atazindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi 17, Zanzibar.

Comments

Popular posts from this blog

CCM YAISHUKURU SMZ, WAKAZI KIKWAJUNI

CCM YAONYA WATEULE MIUNDOMBINU ZANZIBAR

TRA YATAKIWA IJIPANGE DIRA MAENDELEO YA TAIFA